BUKOBA SPORTS

Tuesday, May 8, 2012

STEWART HALL: RUSHWA NDIO KIKWAZO CHA MAENDELEO YA SOKA TANZANIA

KOCHA wa Azam, Stewart Hall amelia na wadau wa Simba na Yanga wanavyoipiga vita timu yake, ambayo imeibuka kuwa kigogo cha Ligi Kuu Tanzania Bara.
Akizungumza na Mwanaposti katika mahojiano maalumu, Hall anasema anashangazwa na mashabiki hasa wa Simba na Yanga kwa kuijengea chuki timu yake kutokana na kutishia ubabe wao.

Hall anaonya kuwa tabia ya wadau wa Simba na Yanga wanaotaka kuona ligi ya Tanzania ikitawaliwa na timu mbili zao tu kitu ambacho si sahihi kwa maendeleo ya soka.

"Timu hizi zimekuwepo kwa miaka mingi sana lakini nashangaa zimeshindwa kusaidia kukuza soka la Tanzania.
"Ninachokiona katika soka la Tanzania kinanisikitisha na kinachonikera zaidi wameingia watu makini wa Azam, ambao wameingiza fedha lakini wanapigwa vita," anasema Hall, ambaye ni raia wa Uingereza.

Anasema Watanzania wanapaswa kuruhusu ushindani na kutolea mfano Ligi Kuu Scotland inavyoshindaniwa na timu mbili tu za Rangers na Celtic na kufanya soka la sehemu hiyo kuwa chini.
Ligi Kuu Tanzania Bara
Hall anasema anafurahia timu yake kushika nafasi ya pili kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara ikiwa miaka chache tangu kuanzishwa kwake.
Anaeleza ni kitu kizuri kuona timu yake iliyoanzishwa mwaka 2004, imeipiku Yanga iliyoasisiwa katika miaka ya 1930.
Azam safari hii imenyakua nafasi ya pili na mwakani itashiriki katika mashindano ya Kombe la Shirikisho.
Hall anaonya Watanzania wanapaswa kubadilika kama kweli wanataka soka la nchi hii ibadilike.
Anasema kuwa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) linatakiwa kuwa makini katika kuendesha katika ligi hiyo.

Analalamikia vitendo vya rushwa kwenye ligi hiyo na viwango duni vya uchezeshaji miongoni mwa waamuzi.
Hall anaeleza kuwa anashangaa kuona rushwa na upangaji matokeo vinakubalika kama sehemu ya soka la Tanzania.

"Ni hatari kwa soka la nchi yenu kama mtakubali masuala ya upangaji matokeo," anasema Hall, ambaye timu yake ililazimika kurudiana na Mtibwa kwenye mzunguko wa pili baada ya mechi ya kwanza kukatizwa kutokana na makosa ya mwamuzi Rashid Msangi.

Pia mechi za Yanga na Polisi Dodoma zilimalizika kwa waamuzi kupigwa kutokana na timu hizo kudai mwamuzi alikuwa anaibeba Azam.

Kocha huyo anakanusha vikali madai hayo na kudai kuwa watu wanaionea wivu tu timu yake kutokana na kuwa na fedha nyingi.
Hall anasema TFF kwa kushirikiana na wadau wa soka la Tanzania wanapaswa kupiga vita kwa nguvu zote masuala ya rushwa.
Anatahadharisha ni ndoto kwa timu za Tanzania kufanya vizuri kwenye michuano ya kimataifa kama wadau wa soka watakumbatia rushwa kama sehemu ya soka la Tanzania.
Anasema wapangaji matokeo wanapaswa kuchukua hatua kali kama Marseille ya Ufaransa ilivyoadhibiwa mwaka 1993 baada ya kubainika ilikuwa inanunua baadhi ya mechi za Ligi Kuu Ufaransa au ile kashfa ya upangaji matokeo ya Italia iliyokuja kujulikana kwa jina la Calciopoli.
Anaonyesha kuwa ubaya wa timu kununua mechi unasababisha Tanzania kuwakilishwa na timu dhaifu kwenye michuano ya Afrika.
"Bwana mwandishi jiulize, timu gani ya Tanzania imetwaa kutwaa taji la Afrika? Jibu linafahamika na ni wazi kuwa linasababishwa na rushwa ndani ya Ligi Kuu," anaeleza Hall, ambaye amewahi kuwa Mkurugenzi wa Ufundi wa Birmingham.

No comments:

Post a Comment