BUKOBA SPORTS

Thursday, August 18, 2016

LIVERPOOL KUCHEZA MECHI ZAKE ZA MWANZO WA LIGI 3 UGENINI MFULULIZO KUPISHA UJENZI WA UWANJA WAO KAMA WALIVYOOMBA.

LIGI KUU ENGLAND ilianza rasmi Msimu mpya wa 2016/17 Wikiendi iliyopita na Liverpool walicheza Ugenini huko Emirates Jijini London na kuitandika Arsenal 4-3.
Mechi 3 zinazofuata kwa Liverpool zote ni za Ugenini.
Kulikoni Liverpool wasicheze kwao Anfield kwa Mwezi mzima na kucheza Mechi 3 za Ligi mfululizo Ugenini kitu ambacho si cha kawaida.
Mechi inayofuata kwa Liverpool ni hapo Jumamosi ikiwa ni Ugenini tena na Burnley na hilo ni kwa makusudi tu kutokana na maombi yao wenyewe ili kupisha kukamilika kwa ujenzi wa upanuzi wa Jukwaa Kuu la Uwanja wao wa Anfield.

Jukwaa hilo limepanuliwa na kuongezwa Ngazi 3 juu za kukalia Washabiki, kupanua Ukumbi wa Wachezaji kuingia na kutoka Uwanjani kutoka Vyumba vya Kubadili Jezi, Mabenchi ya Wachezaji wa Akiba na Jopo lao la Ufundi kutengenezwa upya, sehemu maalum kwa Walemavu na kuboreshwa kwa miundo mbinu ya Watazamaji.

Jukwaa Kuu la Anfield litaongeza Viti 8,500 na kuufanya Uwanja huo sasa upakie Watazamaji 54,000.
Mechi ya kwanza kabisa kwa Liverpool kukanyaga Uwanjani kwao Anfield Jijini Liverpool Msimu huu mpya ni Septemba 10 wakiwavaa Mabingwa Watetezi Leicester City kwenye Mechi ya Ligi Kuu England, EPL na hiyo itakuwa mara ya kwanza Jukwaa Kuu Anfield ‘jipya’ kutumika.

No comments:

Post a Comment