BUKOBA SPORTS

Friday, September 7, 2012

TIMU YA MGAMBO SHOOTING KUJIPIMA KWA MTIBWA SUGAR TANGA KESHO

TIMU ya Mgambo Shooting kesho itapambana na Mtibwa Sugar katika mchezo wa kirafiki utakaofanyika kwenye Uwanja wa Mkwakwani, Tanga.
Meneja wa Mgambo Shooting, Denis Mwingira alisema jana kuwa mchezo huo wa kirafiki utakuwa maalumu kwa ajili ya kuwapima wachezaji waliosajiliwa katika timu hiyo kabla ya kuanza kwa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.
“Licha ya kuwa tumecheza michezo ya kirafiki na timu za majeshi kule Kibaha, lakini tunahitaji michezo mingine ili kuwapa mazoezi zaidi wachezaji wetu,” alisema Mwingira.

Naye kocha wa Mgambo Shooting, Stephen Matata alisema bado ana kazi kubwa ya kukinoa kikosi chake ili kimudu mikikimikiki ya Ligi Kuu inayoanza Septemba 15 mwaka huu.
“Timu yangu ina changamoto ya kuwa na wachezaji wasio na uzoefu wa Ligi Kuu, lakini ni wazuri na wana ari kubwa hivyo ninachofanya ni kuwajenga ili wawe na stamina,” alisema Matata.

Aliwaomba wapenzi wa soka wa Mkoa wa Tanga kuichukulia Mgambo Shooting kuwa ni timu yao kama ilivyo Coastal Union na waiunge mkono vilivyo kwani itacheza soka la kuwafurahisha na kukidhi kiu yao.
“Kuna manufaa makubwa kuwa na timu mbili za Ligi Kuu katika mkoa mmoja, manufaa hayo ni kwamba wapenzi wa soka wataona mechi nyingi kwenye uwanja wao wa Mkwakwani,” alisema Matata.

No comments:

Post a Comment