Sir Alex Ferguson ametoa hongera kwa Mahasimu wao Manchester City kwa leo kutwaa Ubingwa wa Ligi Kuu England Msimu huu baada ya kufungana Pointi na Manchester United lakini wao kubeba Kombe kwa ubora wa tofauti ya magoli.
Huu ni Ubingwa wa 3 katika historia ya Man City baada ya kuutwaa Mwaka 1936/7 na 1967/8 na leo waliutwaa katika Dakika 2 za mwisho za majeruhi baada ya kuzinduka toka bao 2-1 nyuma na QPR na kushinda bao 3-2 na hivyo kuwapiku Man United waliokuwa wameifunga Sunderland 1-0.
Endapo Manchester United wangetwaa Taji leo hili lingekuwa Taji lao la 20 katika historia yao na la 13 tangu Ligi Kuu England ianzishwe Mwaka 1992/3.
Kwa Man City hii ni mara ya kwanza kutwaa Ubingwa wa Ligi Kuu na Timu nyingine zilizowahi kuwa Mabingwa ni Blackburn Rovers, ambao Msimu huu wameshuka Daraja, mara moja, Arsenal, mara 3, na Chelsea, mara 3.
Sir Alex Ferguson amenena: ‘Tumekuwa na wakati mzuri! Tulishawahi kutwaa Taji mara 3 Siku ya mwisho na leo bado kidogo iwe hivyo tena. Kwa niaba ya Manchester United natoa pongezi kwa jirani zetu. Ni kitu kikubwa kutwaa Ubingwa wa Ligi Kuu. Hii ni Ligi ngumu Duniani na yeyote anayeshinda anastahili hilo!’
Aliongeza: ‘Tunakubali changamoto, sisi wazuri kwa hilo na tumeshindana na wapinzani wengi kwa muda mrefu!’
No comments:
Post a Comment